Thursday, 2 October 2025

RC IRINGA ATAKA VIONGOZI KILOLO WASIMAMIE KIKAMILIFU MIRADI YA SERIKALI

 







Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Kheri James, amewataka viongozi wa Halmashauri ya Wilaya ya Kilolo, hususan idara ya elimu sekondari, uhandisi na manunuzi, kusimamia kwa umakini na weledi miradi ya serikali ili kuhakikisha inaleta manufaa kwa wananchi.

RC James alitoa kauli hiyo jana baada ya kutembelea na kukagua miradi mbalimbali ya maendeleo wilayani humo, ikiwemo ujenzi wa mabweni mawili ya wanafunzi wa kidato cha tano na sita katika Shule ya Sekondari Ifingo, Kata ya Kising’a, Tarafa ya Kilolo, kupitia mradi kuboresha mazingira elimu sekondari (SEQUIP).

Katika ukaguzi huo, Mkuu wa Mkoa hakuridhishwa na kasi ya utekelezaji pamoja na usimamizi wa mradi huo, baada ya kubaini kuwa licha ya fedha kutolewa, bweni moja bado halijakamilika.




“Sijaridhishwa na usimamizi wa ujenzi wa mabweni haya. Fedha hazijatumika ipasavyo na baadhi ya majengo yamebaki magofu. Hatutamvumilia mtu yeyote atakayechezea fedha za serikali,” alisisitiza RC James.

Amesema Wilaya ya Kilolo imekuwa ya mwisho katika utekelezaji wa miradi ya kijamii kutokana na upungufu wa usimamizi, ukosefu wa weledi katika uhandisi na manunuzi, hali inayosababisha miradi mingi kuchelewa kukamilika huku wananchi wakikosa huduma stahiki.

“Kila mradi Kilolo unachunguzwa na TAMISEMI, TAKUKURU, lakini bado changamoto ni kubwa. Huu ni uzembe usiokubalika kwa kuwa wilaya hii ina uwezo wa kiuchumi wa kutosha,” aliongeza kwa msisitizo.

Katika ziara hiyo, RC James alikagua pia miradi mingine ikiwemo Kituo cha Afya Nyalumbu, Shule ya Wasichana ya Mkoa wa Iringa (Lugalo Girls High School), Shule ya Sekondari Kilolo, Shule ya Sekondari Lukosi na Kituo cha Afya Ruahambuyuni.

WITO KWA WANANCHI IRINGA

Wakati huohuo, Mkuu wa Mkoa wa Iringa aliwataka wananchi wa Kata ya Magulilwa, Tarafa ya Mlolo, Wilaya ya Iringa, kulinda na kutunza miundombinu ya Kituo cha Afya Mlanda ili kiweze kutoa huduma bora kwa muda mrefu.





Alisema mafanikio ya miradi ya maendeleo yanategemea sio tu serikali na wataalamu, bali pia ushirikiano wa wananchi katika kuitunza na kuilinda.

“Kituo hiki ni cha wananchi wote. Ni wajibu wetu kukilinda dhidi ya uharibifu wa aina yoyote. Tunahitaji usimamizi madhubuti kutoka kwa wataalamu na ushirikiano kutoka kwa jamii,” alisema RC James.

Aidha, aliwataka wataalamu wa halmashauri zote kuhakikisha wanatekeleza majukumu yao kwa weledi na uadilifu, sambamba na kuhakikisha thamani ya fedha inaonekana kwenye kila mradi unaotekelezwa.

Ziara hiyo ni sehemu ya mikakati ya Serikali ya Mkoa wa Iringa katika kufuatilia kwa karibu utekelezaji wa miradi ya maendeleo na kuhakikisha huduma za msingi kama elimu na afya zinawafikia wananchi kwa ubora unaostahili.

Mwisho


No comments:

Iringa Regional Commissioner Calls On Kilolo Leaders To Strictly Supervise Government Projects

IRINGA – The Iringa Regional Commissioner, Kheri James, has urged leaders of the Kilolo District Council—particularly those in the secondary...