IRINGA WAANZA MAANDALIZI YA MPANGO MKAKATI WA KUTOKOMEZA UKATILI WA KIJINSIA
Iringa. Katika
juhudi za kupunguza vitendo vya ukatili wa kijinsia (GBV), Mkoa wa Iringa kwa
kushirikiana na wadau mbalimbali umeanza kuandaa rasimu ya utekelezaji wa
Mpango Mkakati wa Taifa wa Kutokomeza Ukatili dhidi ya Wanawake, Watoto na
Wanaume (MTAKUWA II) ngazi ya mkoa, kwa lengo la kuhakikisha ukatili unatokomezwa
kwa kiwango cha juu kabisa.
Kikao kazi cha
maandalizi ya mpango huo wa kitaifa wa miaka mitano (MTAKUWA II 2024/25 –
2028/29), kiliongozwa jana na Kaimu Katibu Tawala wa Mkoa wa Iringa, Saida
Mgeni, ambaye pia ni Mkuu wa Kitengo cha Maendeleo ya Jamii mkoani humo.
Afisa Maendeleo ya
Jamii na Mratibu wa MTAKUWA/NPA-VAWC mkoa wa Iringa, Grace Simalenga, alisema
mpango mkakati wa awamu ya pili umejumuisha pia wanaume na wavulana ili
kuhakikisha mapambano dhidi ya ukatili yanagusa makundi yote.
“Leo tumekutana
kupitia maandalizi ya mpango mkakati wa mkoa kwa ajili ya kupambana na ukatili
dhidi ya wanawake, watoto, wanaume na wavulana. Tulihusisha waratibu wa
halmashauri, viongozi wa dini, taasisi mbalimbali, pamoja na waandishi wa
habari ili kuhakikisha mpango huu unatekelezeka kwa ufanisi,” alisema
Simalenga.
Aliongeza kuwa
kikao hicho kimewezeshwa na Shirika la SOS Children’s Villages kupitia
ushirikiano wa serikali na sekta binafsi (PPP). Shirika hilo limekuwa mstari wa
mbele katika kupinga mimba za utotoni na kuwawezesha wasichana waliojaliwa
watoto wakiwa katika umri mdogo.
Meneja Miradi wa
SOS Mkoa wa Iringa, Victor Mwaipungu, alisema shirika hilo limeamua kuunga
mkono juhudi za serikali kwa kujenga uwezo wa kamati za MTAKUWA II kuanzia
ngazi ya mkoa, halmashauri hadi kata.
“Kamati hizi
zikijengewa uwezo na uelewa wa kutosha kuhusu maeneo ya kipaumbele ya MTAKUWA
II, mapambano dhidi ya ukatili yatakuwa rahisi na yenye tija,” alisema
Mwaipungu.
Kwa upande wake,
Mchungaji Upendo Koko kutoka KKKT Dayosisi ya Iringa, ambaye pia ni Mwenyekiti
wa Idara ya Wanawake na Jinsia kwa Jumuiya ya Makanisa ya Kikristo Tanzania
mkoani Iringa, alisema rasimu hiyo ikikamilika itasaidia kupunguza kwa kiasi
kikubwa vitendo vya ukatili katika jamii.
Naye Mrakibu Msaidizi
wa Polisi na Mkuu wa Dawati la Jinsia na Watoto mkoani Iringa, Elizabeth Swai,
alisema jukumu kubwa la wajumbe wa kamati hiyo ni kutoa elimu na kuhakikisha
makosa yote yanayohusiana na ukatili wa kijinsia yanashughulikiwa ipasavyo.
Aidha, Afisa Ustawi
wa Jamii na Mratibu Mwenza wa MTAKUWA II mkoa wa Iringa, Martin Chuwa, alisema
mpango mkakati wa awamu ya pili umeboreshwa kwa kuongeza maeneo mapya, ikiwemo
ukatili wa kimtandao na kuhusisha zaidi wanaume na wavulana.
“Takwimu zinaonesha
kuwa ukatili dhidi ya wanaume nao unaongezeka mwaka hadi mwaka. Pia mpango huu
umeongeza ushirikiano wa taasisi binafsi katika nafasi za uratibu,” alisema
Chuwa.
MTAKUWA wa awamu ya
kwanza ulikamilika, na sasa awamu ya pili (MTAKUWA II) inaanza kutekelezwa kwa
kipindi cha miaka mitano, 2024/25 – 2028/29, kwa lengo la kuhakikisha Tanzania
inakuwa taifa lisilo na ukatili wa kijinsia.
Mwisho
No comments:
Post a Comment