Monday, 15 September 2025

MASHABIKI WA SIMBA NA YANGA WATOA TAMBO KUELEKEA NGAO YA JAMII


Iringa — Shamrashamra na tambo za soka zimechukua nafasi leo katika mtaa wa Mantigo, kata ya Miyomboni, Manispaa ya Iringa, baada ya mashabiki wa timu hasimu za Simba SC na Yanga SC kukutana na kushindana kwa kauli kuelekea pambano la watani wa jadi litakalohusisha pia Ngao ya Jamii, kuashiria mwanzo wa msimu mpya wa Ligi Kuu NBC Tanzania Bara 2025/2026.

Mashabiki hao walisisitiza kuwa mechi hiyo itakuwa kivutio kikubwa si tu kwa wakazi wa Iringa, bali pia wageni kutoka mikoa jirani, huku kila upande ukijiamini kutwaa ushindi na kutoa taswira ya mwelekeo wa msimu mpya.

“Msimu huu Simba haiwezi kufungwa, tunakuja kuchukua alama tatu muhimu Iringa,” alisema kwa kujiamini David Bovansi, shabiki kindakindaki wa Simba SC.

Upande wa Yanga nao ulijibu mapigo.

“Yanga ni bingwa wa kweli, tutathibitisha uwanjani kwamba tunastahili kubeba tena taji la Ligi Kuu,” alisema Boniface Makunga, mwenyekiti wa tawi la Yanga Manispaa ya Iringa.

Zaidi ya tambo na ushindani wa uwanjani, mashabiki hao walibainisha kuwa tukio hilo litakuwa na manufaa ya kiuchumi kwa wakazi wa Iringa kupitia biashara ndogondogo zitakazoibuka kutokana na ujio wa mashabiki kutoka ndani na nje ya mkoa.


 

No comments:

MASHABIKI WA SIMBA NA YANGA WATOA TAMBO KUELEKEA NGAO YA JAMII

Iringa — Shamrashamra na tambo za soka zimechukua nafasi leo katika mtaa wa Mantigo , kata ya Miyomboni , Manispaa ya Iringa, baada ya mash...