Monday, 15 September 2025

SALIM ABRI (ASAS) AIZINDUA KAMPENI ZA CCM KILOLO, AMTANGAZA DR. RITTA KABATI


Kilolo, Iringa – Septemba 14, 2025

Mjumbe wa Kamati Kuu ya CCM Taifa (MCC) na Mratibu wa Kampeni Kanda ya Nyanda za Juu Kusini, Salim Abri maarufu kama Asas, leo amezindua rasmi kampeni za Mgombea Ubunge wa Jimbo la Kilolo pamoja na wagombea wa nafasi za udiwani kupitia CCM katika jimbo hilo.

Mgombea Ubunge wa Kilolo, Dr. Ritta Kabati, ndiye mwanamke pekee kati ya wagombea wa majimbo saba ya ubunge mkoani Iringa kupitia CCM. Akizungumza wakati wa uzinduzi huo, Dr. Kabati aliishukuru CCM kwa kuendelea kumuamini na kumpa jukumu la kupeperusha bendera ya chama, akisisitiza kuwa uzoefu wake wa miaka 15 kama Mbunge wa Viti Maalum umemwandaa vyema kuwatumikia wananchi wa Kilolo kwa bidii, uadilifu na upendo.

Ameahidi kutekeleza kikamilifu Ilani ya CCM 2025–2030 bila upendeleo, huku akihimiza mshikamano kati ya viongozi na wananchi, kuvunja makundi ya kijamii na kisiasa, na kuharakisha maendeleo ya jimbo hilo. Aliwaomba wananchi kumpigia kura yeye, Rais Samia Suluhu Hassan na madiwani wote wa CCM.

Kwa upande wake, Salim Abri (Asas) alisema Dr. Kabati si mgeni katika uongozi, akibainisha kuwa Kilolo imepata mgombea mwanamke mwenye maono, uzoefu na uwezo wa kushughulikia changamoto za wananchi. Alisisitiza kuwa Dr. Kabati amejikita katika kupigania huduma bora za afya, upatikanaji wa maji, kupambana na rushwa, na kusaidia makundi maalum kama watu wenye ulemavu.





Aidha, Abri alitaja baadhi ya mafanikio yaliyopatikana Kilolo chini ya Serikali ya Awamu ya Sita, yakiwemo ujenzi wa vituo vya afya vitano, zahanati kumi, vyumba vya madarasa 493, vyoo 352, miradi ya maji safi, pamoja na shule ya sekondari ya wasichana ya mkoa. Alisema mafanikio hayo ni ushahidi wa utekelezaji bora wa ilani ya CCM unaoendelea kuleta matokeo chanya kwa wananchi.

Mwenyekiti wa CCM Wilaya ya Kilolo, John Kiteve, alisema wananchi wa Kilolo wako tayari kuiunga mkono CCM kwa kura zote, akibainisha kuwa ilani ya mwaka 2020–2025 imetekelezwa kwa mafanikio makubwa katika sekta mbalimbali, huku ilani ya 2025–2030 ikilenga zaidi kutatua changamoto za wananchi na kuboresha maisha yao.




 

No comments:

SALIM ABRI (ASAS) AIZINDUA KAMPENI ZA CCM KILOLO, AMTANGAZA DR. RITTA KABATI

Kilolo, Iringa – Septemba 14, 2025 Mjumbe wa Kamati Kuu ya CCM Taifa (MCC) na Mratibu wa Kampeni Kanda ya Nyanda za Juu Kusini, Salim Abri...